Jinsi ya Kuandika Riwaya/Hadithi

Jinsi ya Kuandika Riwaya/Hadithi

Jinsi ya Kuandika Riwaya/Hadithi

UANDISHI wa Riwaya ni fani ya usanii kama fani zingine za uandishi kama vile Uandishi wa Habari, Uandishi wa Vitabu vya Taaluma, Uandishi wa Majarida, Uandishi wa Sinema, nakadhalika.

Uandishi wa riwaya unazo taratibu na kanuni zake ambazo mwandishi anapozifuata ataweza kuandika hadithi za kuvutia, zenye mafunzo na hata kuweza kuzikamilisha katika muda mfupi pasi na kuathiri shughuli zake; kwamba, kuweza kwake huko si lazima awe amekwenda chuo cha uandishi, ila kuwa na elimu ni msaada zaidi katika kurahisisha mambo kwa tafsiri ya kukuweka katika upeo mpana wa uono. Hatahivyo, pamoja na kutokwenda chuo kwa mwandishi, bado anapaswa kujua kanuni za uandishi husika ili kuwa mwandishi bora.

KWANINI MTU ANAANDIKA HADITHI?

Mosi – mtu uandika ili kutoa hisia zake juu ya jambo au tukio fulani kwa jamii pasi na kutarajia malipo.
Mbili – mtu uandika ili kuendeleza utamaduni au simulizi za waandishi waliopita.
Tatu – mtu uandika kama sehemu yake ya maisha katika kujipatia kipato.
Nne – mtu uandika kwa sababu za kitaaluma au kama mtihani.

HATUA ZA KUFUATA
1. Chagua somo

2. Jiulize: je, nina utaalam wa somo hilo? Kama sina – je, nipo tayari kujifunza ili kutekeleza azma yangu?

3. Kumbuka kuwa, kuandika ni pamoja na kuelewa nini unataka kuandika.

4. Chagua mwanzo.

5. Chagua mwisho-
Kwa kuchagua mwanzo na mwisho, mwandishi anapata dira ya mwelekeo wa hadithi badala ya ‘kuogelea kwenye bahari ya matukio mengi’ huku mengine yakiwa hayahusiani na hadithi.

6. Hapa katikati chagua mgongano wa mawazo, Ndiyo/Hapana, Furaha/Huzuni, Amani/Ugomvi, Dini/Ukafiri, Chama kimoja/Vingi, Ukuwadi/Uungwana, nakadhalika.
Pendekeza mahali ambapo hadithi itahusishwa – Mjini?/Kijini?, Tanzania?/Kwingineko?, Mchanganyiko?

7. Chagua wawakilishi wakuu na uwape majina na sifa (Elimu, sura, tabia, n.k.): mhusika mkuu (nyota) atakayekuwa toka mwanzo hadi mwisho; mhusika wa akiba kama hutaki mhusika mkuu afike mwisho; mhusika mkuu mkinzani atakayekuwa mwanzo hadi mwisho; mkinzani wa akiba kama hutaki mkinzani mkuu afike mwisho.
Tengeneza fremu ya hadithi: mfano, sura ya 1, 2, 3, 4…na sura ya mwisho; hitimisha kulingana na mgongano wa mawazo uliojitokeza hadithini.

Jinsi ya Kuandika Riwaya/Hadithi

Jinsi ya Kuandika Riwaya/Hadithi

Andika kwa undani sura mojamoja – fanya utafiti kwa kila tukio unalotaka kuandika ili uwe na hadithi ya kuaminika au inayoonekana ya kuaminika hata kama ni riwaya.

Ondoa mawazo potovu: kumbuka mwandishi ni kioo cha jamii – maandishi yako yanakuwa fundisho kwa wengine, ukiandika ya kupotosha jamii itapotoka, kwa maana kalamu ni kali kuliko upanga maana unaweza kulaumiwa kama sio kujikuta ukilaaniwa!

8. Piga chapa/taipu muswada ghafi – ni vyema kwa kutumia kompyuta katika zama hizi za tekinolojia ya elektroniki.

9. Chapa (print); soma na kufanya masahihisho ya awali.

10. Rekebisha makosa.

Inapendekezwa sana kufanya masahihisho mwenyewe kama unajua kutumia kompyuta kwakuwa ni rahisi kuongeza/kuondoa mawazo na kuharakisha kukamilika kwa muswada (tuwasifu waandishi wa zamani ambao walifanya yote kwa mkono zaidi)

Wakati wa kufanya masahihisho, usiishie kusahihisha makosa tu, bali ‘uisikilize’ hadithi na kupata mantiki.
Ukipata wazo jipya na bora zaidi usisite kuliweka.

Fanya hivi sura moja hadi nyingine huku ukihakikisha kila sura inajitegemea katika kupeleka ujumbe wake (usirudie jambo lililokwishazungumziwa nyuma)

Angalia: je, lengo lako la kumalizia limebakia kama mwanzo au mawazo mapya yamelibadilisha? Kama limebadilika kulingana na taarifa mpya, kubali mabadiliko kwani riwaya siyo msahafu!
Angalia upya jina la kitabu: je, linaendana na riwaya pamoja na umaliziaji? Kama halilingani, chagua lingine maramoja!

11. Chapa tena. Soma muswada wote na kufanya masahihisho kwa mkono.

12. Yahawilishe masahihisho ya mkono kwenye mashine.
Hatua hii pia inashauriwa kuifanya mwenyewe badala ya kumpatia mpiga chapa kwakuwa inakusaidia ‘kufinyanga maandishi mweyewe’ pindi ukipata kosa au kujiwa na wazo jipya.

Tangu mwanzo hakikisha unatunza kazi yako isipotee. Weka nakala katika ‘cd’ zaidi ya moja mbali na ile ya kompyuta yako. Ikiwezekana azima nafasi kwenye kompyuta ya mwenzio kujikinga iwapo yako itaharibika na taarifa zote kupotea.
Usitupe kazi yako ya mwanzo kwakuwa inayo nafasi kubwa ya kuja kukusaidia pindi ukipotea njia.

13. Chapa tena.

14. Hii ni hatua muhimu sana kuliko zote: Soma hadithi yote KAMA VILE NI YA MTU MWINGINE:
Hapa unakuwa mhariri mwenyewe. Kosoa bila huruma na kutoa maoni kwa madhumuni ya kuiboresha.
Jifanye wewe ndiye msomaji: kumbuka kwamba Mambo anayopenda mwandishi si lazima msomaji ayapende. Kwa kujifanya msomaji tofauti na mwandishi utaweza kugundua kasoro ndani ya hadithi. Katika hatua hii, ni vyema ukaipitia hadithi baada ya muda mrefu tangu uikamilishe; kwani kwa kufanya hivyo katika kuipatia muda, ndivyo unaipatia muda akili yako (wakati huo itakuwa umepoa) kuondokana na kujipendelea kwakuwa hakukusaidii katika uandishi.

Fanya utafiti wa ziada unapokuwa na wasiwasi.

Rekebisha makosa kwa mara ya mwisho. Angalia mantiki, miundo ya sentensi, misemo, nakadhalika.

15. Mpatie mtaalam kazi ya kuupitia muswada kikamilifu ikiwa ni pamoja na kurekebisha muundo na mantiki. Huyu ni mtu muhimu sana kwakuwa anakuwa kama msaidizi wako huku ukitambua kuwa si lazima ukubaliane na mawazo yake hata kama jambo moja linabakia kuwa bayana kwamba hadithi ni yako yako tu (hapa nasisitiza, usikubali itekwe nyara na mwingine maana si yake ingawaje hoja inashika kwamba mara nyingi anayokueleza huwa ndiyo sahihi kuliko hata ufikiri wako, hivyo usiwe mgumu kubadilika! Ila hatushauri ukubali kuburuzwa, mwandishi mbishi ni mzuri zaidi, lakini mwandishi aambiliki ni rahisi zaidi kuburuzwa na upumbavu wake)

Ndio, mtaalamu huyu ni mkatishaji tama maana hana simile katika kudhihirisha kile anachokiona si sahihi au ni utumbo! Huyu ni myekaji kila mahali, anaweza kufyeka asibakishe kitu katika huko kuandika kwako maana anaweza kuuchafua muswada kiasi cha kukufanya hata ushindwe kujiamini na kujiona pengine umevamia fani!

Yupo mtu mwingine unayepaswa pia kumpatia kazi yako; hatahivyo huyu si kama huyo wa awali ambaye ni ‘katili’, huyu ni wa kukupatia maoni tu. Mara nyingi huyu ni mkosoaji tu wala hakusaidii sana kuandika hadithi yako maana yeye huifanya kazi yake akidhani wewe unazijua kanuni kiasi akigundua kosa au makosa anaweza kushangaa ni kwa nini ufanye makosa ya kimsingi! Huyu hufikiri hadithi yako imekamilika kumbe mara nyingi sivyo.

Hivyo ni jitihada zako tu za kumuelewa anachotaka ndizo zitakazokufanya kutekeleza yale anayokuagiza; huyu kwa tafsiri nyingine ni mwalimu wako ukiwa kazini, ndiye atakayeifanya hadithi yako iwe ‘hadithi’ maana likitajwa jina lake (mtu huyu anaipenda sana lugha iliyonyooka) katika walioupitia muswada wako una uhakika wasomaji watakikimbilia kitabu chako mara kitakapokuwa kimechapishwa na kuwekwa sokoni. Ikiwezekana mwambie akurekebishie maeneo yenye makosa kimuundo, ikiwa ni pamoja na kuandika upya aya au sura nzima (usisahau utatakiwa kuongeza posho maana si rahisi watu hawa kukufanyia kazi bure hasa katika zama hizi za kila kazi ni biashara!)

16. Tafuta mshauri wa kukuelekeza ni kampuni gani itaipokea aina hiyo ya hadithi; ila mara nyingi wataalamu wote wawili hapo juu wanawajua wachapishaji hao.

17. Tamati.

Imeandaliwa na Shaaban Mngazija

Je, unakubaliana na maelezo haya?

13 thoughts on “Jinsi ya Kuandika Riwaya/Hadithi

  1. Nakubaliana na maoni haya kwa kiasi Fulani,kwani bado sijabobea sana katika fani hii,ila ningependa kuomba msaada na mwongozo was jinsi ya kuandika riwaya kwani mie ni mpenda fasihi

  2. nilianza kuandika riwaya yangu mwaka uliopita mwezi wa sepetemba niko sura ya sita lakini nina hofu mswada wangu unaweza ibiwa wakati wa kuuhariri aukuuchapisha,,,, nina pania kuwa mwandishi,,,, mnaweza nipa mawaidha yepi?

  3. nimeandika mswada wangu ila nimekosa mahali pa kuanzia .Mashahiri yangu na akili zangu za kifasihoi zinalala kwenye makasha.Iwapo naweza kumpata mwelekeze mwenye mawazo chanya ya kunisaidia basi sina radhi…………

Leave a comment